“Yafueni majembe yenu yawe panga, na miundu yenu iwe mikuki; aliye dhaifu na aseme, Mimi ni hodari”, Yoe 3:10 SUV.

Mtu aliyechoka sana kwa kukata tamaa au kwa kuchoka, mtu huyu anaweza kuinuliwa kwa kinywa chake mwenyewe, ama mtu huyu anaweza kuinuliwa na maneno yenye kumtia moyo.

Ukiri wa mtu kupitia kinywa chake una nguvu nyingi sana za kumfanya ajione jasiri, shujaa, hodari, ajione anaweza kufanya jambo alilolikatia tamaa, ajione anaweza kuinuka tena.

Tunaweza kusema kinywa kimebeba ushindi wa mtu, na kimebeba kushindwa kwa mtu, mtu akikiri ushindi atashinda, mtu akikiri kushindwa atashindwa, mtu akikiri kupona atapona, mtu akikiri kutopona itakuwa hivyo.

Kinywa cha mtu kwa maana nyingine kimebeba hatima ya maisha ya mtu, mtu anapojitamkia mema anaumba kitu ndani yake, ambacho hicho kitu kitatokea katika mazingira yanayoonekana kwa macho ya nyama.

Yapo mazingira magumu sana tunaweza kujikuta tumo humo, wale wanaojiona watu wa kufa na wanakiri kwa vinywa vyao, watu hao mara nyingi wanavuna matunda ya ukiri wao, watu wanaokiri ushindi katikati ya magumu mara nyingi huimbuka washindi.

Kwanini inatokea hivyo, hii inakuwa hivyo kwa sababu mtu anakuwa kama vile amejiambia nipo tayari kufa, na mwingine anakuwa amejitamkia sipo tayari kufa kwenye hii hali ngumu ninayokutana nayo.

Vita vyetu vingi tunaweza kushinda kutokana na vile tunavyokiri, hali nyingi za maisha tunaweza kuibuka washindi kutokana na ukiri wetu, ukiri wetu unatuonyesha vile imani yetu ilivyo kwa kiwango gani kwa Mungu wetu.

Mtu anapojiona hawezi kushinda vita fulani, maana yake ameona hata Mungu aliyenaye hawezi kumsaidia jambo lolote kwenye maisha yake au kwenye hali anayopitia wakati huo.

Neno hili katika biblia linatufunza mengi sana “aliye dhaifu na aseme, Mimi ni hodari”, Yoe 3:10(b) SUV. hakusema aliye dhaifu ajione yeye hatahusika chochote na ajione ni mtu wa kufa tu, kumbe huyo huyo aliyekuwa anajiona hawezi ajione anaweza.

Hata kwako leo kiri kwa kinywa chako kuwa unaweza, wewe ni mshindi/hodari kwenye pito unalopitia kwenye maisha yako, kukiri kwako unainua imani ya Kimungu ndani yako, utaanza kuona mambo kwa sura au  mtazamo tofauti kabisa.

Mungu akubariki sana

Samson Ernest

+255759808081