Nakusalimu katika jina la Bwana wetu Yesu Kristo aliye, siku nyingine tena mpya kabisa Bwana ametupa kibali cha kuiona. Sifa na utukufu tumrudishie yeye Bwana mwenza wa yote, anayetupa uzima kila iitwapo leo.
Wakati naanza kusoma agano la kale, kuna maeneo yalikuwa yanipa shida, nikijiambia niruke kusoma hayo maeneo au nifanyaje. Nikakumbuka napaswa kusoma na kutoa tafakari yangu kutokana na jinsi tulivyojiwekea taratibu zetu za kikundi za kusoma sura husika na kutoa kile umejifunza kupitia sura hiyo.
Nilichoona hayo maeneo hayana maana kwangu kuyasoma, yaani kama vile niliyaona hayawezi kunisaidia chochote. Mfano unakuta sura nzima inataja ukoo wa fulani au fulani baba yake alikuwa fulani. Hapo naona kama vile kwangu inanikuzaje kiroho, nikasahau na hayo ni maandiko matakatifu.
Wakati naendelea kupata shida kuhusu hilo huku nikiangalia tumewekeana na wenzangu lazima tusome sura husika na tutoe tafakari zetu. Nilijikuta nakubaliana na hiyo hali, bahati nzuri nikapata amani moyoni kwa kusikia kusoma kila kitu ili kufahamu zaidi uzao fulani ulitokana na nani.
Baada ya kulijua hilo, nilianza kupenda kusoma biblia kwa amani na kufurahia kile nasoma, kule kupuuzia na kuona haina maana kukatoweka kabisa. Nikaona kumbe kuna vitu vingine huwa tunavipuuza lakini vina maana kubwa sana katika maisha yetu ya kujifunza Neno la Mungu.
Ikanifunza jambo lingine la msingi sana, kutopuuza andiko lolote lenye pumzi ya Mungu. Chochote kilichoandikwa kwenye biblia yako, kina maana kubwa sana, sio maana kubwa tu. Kinaweza kukusaidia kukua katika eneo ambalo unahitaji ukue hata usipoelewa wakati huo, kujua uzao wa fulani ni faida kwako mkristo unayefuatilia vitu.
Unapojifunza Neno la Mungu, usichague vitu vya kujifunza, weka utaratibu wa kusoma biblia yako hatua kwa hatua. Acha ile tabia ya kuruka baadhi ya sura, ukiona sura fulani haina maneno malaini na matamu unaamua kuiruka. Hiyo haitakufikisha kwenye viwango ya juu vya ukomavu wa kiroho.
Kila Neno la Mungu lililoandikwa ndani ya biblia, linafaa wa mafundisho, kama linafaa kwa mafundisho. Maana yake linakufaa kukufundisha wewe, hata kama huna tabia fulani mbaya unakuwa unajua jambo fulani ni muhimu kwako kulifanya, na jambo fulani kwako halifai ulifanye.
Unaweza usilione leo lina umhimu kwako, ila itafika kesho utaliona la muhimu. Itakuwa furaha kwako kukutana na kitu ambacho ulishajifunza, unajua matokeo ya kufanya na kutofanya, unajua njia ya kupita na njia ya kuepuka kupita.
Wakati mwingine watu watakuja kuomba msaada kwako kwa hilohilo ulilotaka kulipuuza, wanapokuja kwako inakuwa rahisi kuwasaidia kwa sababu ulishajifunza. Lakini kama hukujifunza utaona Usumbufu kwako, maana hujui chochote kuhusu hilo unaloulizwa.
Usikimbilie mbele, kimbilia kuelewa unachosoma, hakikisha unaposoma Neno la Mungu akili yako inakuwa pale. Usisome Neno la Mungu huku unaweza vitu vingine, hutakaa ufurahie usomaji wako wa Neno la Mungu.
Ukutane na sehemu ina maneno magumu na wakati mwingine unashindwa kuelewa unachosoma, we endelea kusoma hivyo hivyo. Katika sura nzima lazima utapata maneno ya kukujenga, na hayo uliyoona magumu itafika mahali utaanza kuyaelewa.
Biblia pamoja na wengi wanaona ni ngumu, ila naipenda kitu kimoja, maneno mengi yameandikwa kwa kujirudia kwa namna ambayo unaweza kuelewa zaidi pale ambapo ulipata ugumu. Mara chache sana utakutana na habari ambayo haijaandikwa kwenye kitabu kingine.
Usiingiwe na mashaka ukaanza kutamani kuruka baadhi ya vitabu, hiyo kazi waachie wale wanaotafuta njia ya kujizoeza kusoma Neno la Mungu. Lakini wewe uliyeanza kwa muda kusoma Neno la Mungu, hakikisha huruki sura hata moja, utaona faida kubwa sana.
Mungu akubariki sana kwa kutoa muda wako kusoma ujumbe huu, usiache kutembelea mtandao wetu wa www.chapeotz.com kupata masomo mengine mazuri zaidi.
Nakutakia wakati mwema.
Facebook: Chapeo Ya Wokovu
Tovuti: www.chapeotz.com
Email: chapeo@chapeotz.com
WhatsApp: +255759808081.