Kama mtu uliyetulia vizuri, utaona kuna upepo fulani hivi unapita, ambao umewafanya watu kuwa kwenye hali fulani hivi ya sintofahamu. Ukiwa rohoni ndio unaweza kuliona hili jambo kwa upana zaidi, kila mmoja anapita kwenye fulani ambayo hajaizoea kabisa.

Usipokuwa makini na Mungu asipokupa ujasiri wa kusonga mbele, bila kujali hali uliyonayo sasa, nakwambia kuna mambo yatabaki historia kwako. Kuna mambo utaacha kuyafanya kabisa katika maisha yako ya kila siku, unaweza usijione kwa haraka kama unapoteana, ila ukweli utauona kadiri siku zinavyozidi kwenda mbele, unakuwa hufanyi yale ulikuwa unafanya.

Yapo mambo yanayotokea katika maisha yetu, yanatugusa moja kwa moja kwenye uchumi wetu, yanagusa moja kwa moja afya zetu, yanagusa moja kwa moja kazi zetu, yanagusa moja kwa moja masomo yetu, yanagusa moja kwa moja watoto wetu, na yanagusa moja kwa moja familia zetu.

Mambo kama haya niliyokutajia hapo juu, moja wapo likikupata au kama limeshakupata, usipokuwa mwangalifu na stamina za kutosha unaweza kupata mateso makali sana moyoni mwako. Mahangaiko hayo ya moyo yanaweza kukuondoa kwenye ratiba zako zote za kumtukuza Mungu wako.

Unaweza kujiona ghafla hamu ya kusoma Neno la Mungu inatoweka mara moja, utajaribu kujisukuma kwa nguvu kufanya kile ulikuwa unafanya kila siku. Utaona kabisa haupo kama zamani, unaweza kuanza kutafuta shida ni nini, wakati mwingine unaweza kusahau kilichokufanya uwe hivyo ni jambo fulani lililokupa.

Mtu anaweza kukuuliza swali kwa jinsi anavyokuona unazidi kukaa mbali na yale mazuri uliyokuwa unafanya. Unaweza kumjibu huna tatizo lolote, sio kwamba hutaki kumwambia, wakati mwingine unaweza usijue kilicho kufanya uwe hivyo.

Jichunge sana ndugu yangu, jambo lolote linaweza kukutokea likaujeruhi sana moyo wako, usipokuwa mwangalifu kipindi hicho. Usipoachilia hilo lililokupata, nakueleza ukweli kabisa, utaanza kuona hamu ya kuomba inaisha, hamu ya kusoma Neno la Mungu inakatika, na hamu ya kuhudhuria kanisani inapotea kabisa.

Unaweza kuwa umekuwa mvumilivu sana kwa mambo mengi, likakupata jambo moja lenye kukuumiza kiasi kwamba unaona hata ule uvumilivu uliokuwa nao unaondoka. Utatafuta nini imekufanya uwe hivyo, kumbe jambo lililokupata hukujipanga nalo kabisa, maana hukutegemea kama lingekuja kukutokea wewe.

Ulizoea kuona kwa wengine, ulizoea kusikia kwa wengine, wakati mwingine uliona kama ni jambo rahisi kulibeba na kulikubali moyoni mwako. Leo limekutokea wewe, vile ulikuwa unafikiri unaona ipo tofauti kabisa, unashangaa moyo wako unapata maumivu makali sana, kila ukijaribu kujisahaulisha. Na kila ukijaribu kukumbuka mambo mengi uliyovumilia kipindi cha nyuma, unaona kabisa hilo huwezi kuvumilia.

Ukishaona umepatwa na jambo ambalo linaondoa ule uvumilivu na utulivu wako, jitahidi sana usikae mbali na Mungu wako. Usijidanganye kupumzika kwanza mambo ya Mungu, usiseme naacha kwanza kusoma Neno la Mungu hadi pale nitakapokaa sawa. Hebu wewe fikiri, umepita mangapi ya kukuumiza moyo wako, alafu hayo yote hukuwahi kusema unaacha kwanza ratiba yako ya kusoma Neno la Mungu.

Leo limetokea hilo unapata wazo la kuacha kusoma Neno la Mungu, ukirudi nyuma kuna siku ulisema hivyo hivyo unaacha kwanza ratiba yako ya kusoma Neno la Mungu. Ulipata shida sana kurudi tena kwenye ratiba yako ya kusoma Neno la Mungu, leo umepatwa na jambo unaona hiyo hali ya kuacha inakujia tena.

Usikubaliane na hali hiyo, unaweza kuona sijui tu maumivu unayopitia, nakueleza tu ukweli, hakuna maumivu matamu, maumivu yote ni machungu. Inategemeana na wewe vile umejijenga vipi kukabiliana na mambo magumu katika maisha yako. Kusoma kwako Neno la Mungu kunasaidia sana kuwa na mtazamo chanya pale unapokutana na jambo gumu mbele yako.

Ikiwa unasoma sana Neno la Mungu, alafu ndani yako bado umejaa mitazamo hasi, ujue bado ufahamu wako hujafunguliwa. Ungefunguliwa ufahamu wako ungeona mambo kwa namna ya tofauti sana, namna ambayo kwa mtu asiyemjua Mungu wako, ataanza kumtamani na yeye awe naye.

Shika sana haya ninayokueleza hapa, yatakusaidia sana katika safari yako ya wokovu. Hata maisha yako ya kawaida kabisa, itakusaidia kutorudi nyuma, kwa sababu ya mambo yanayokupata katika maisha yako.

Mungu akubariki sana.

Chapeo Ya Wokovu.

Tovuti: www.chapeotz.com

Email: chapeo@chapeotz.com

WhatsApp: +255759808081