
Katika maisha yetu tunapaswa kujifunza kutokuwa mizigo kwa wengine, hata kama tutakuwa tunahitaji sapoti ya wengine katika huduma zetu au katika maisha yetu, hatupaswi kuwalemea sana watu.
Kufanya kazi za mikono kwa bidii inatupasa watumishi wa Mungu, sio kwa kuwa ni watumishi wa Mungu tusifanye kazi, tunapaswa kufanya kazi za mikono yetu.
Kama ni kulima mashamba tunapaswa kulima kwa bidii, kama ni kufanya biashara tunapaswa kufanya kwa bidii, kazi ambazo tutazifanya na tutapata muda wa kwenda kuhubiri injili ya Kristo.
Hatupaswi kabisa kutegemea sadaka za washirika, hata kama wanapaswa kutoa sadaka zao kwa ajili ya kazi ya Bwana, sisi hatupaswi kuishia hapo. Tunapaswa kuwa na shughuli zingine zinazoweza kutuingizia kipato, ili tusiwe tegemezi sana.
Kuna wakati tutapaswa kusafiri kwenda mahali kwa ajili ya injili, ili usiwe mzigo, kuna maeneo itabidi ujihudumie mwenyewe. Maana yapo mazingira ukifika wao wenyewe wanahitaji kusaidiwa kifedha, sasa wewe ukitaka kupata kila hitaji kwao, utageuka mzigo mzito kwao.
Pamoja na tunapaswa kuwekeza muda wetu mwingi kwenye huduma, kuna wakati tunapaswa kuwa kwenye shughuli za kutuingizia kipato. Au unaweza ukawa na mradi wa kukuingizia fedha za kuweza kukusaidia kwenye mahitaji wakati wa huduma, na kuisaidia familia yako.
Hili tunajifunza kupitia maandiko matakatifu, sio jambo ambalo ni la hewani, au sio maneno tu ya kutunga, tunajifunza kupitia maandiko. Watumishi wa Mungu walikuwa wanahubiri injili na kufanya kazi za mikono yao.
Rejea: Maana, ndugu, mnakumbuka taabu yetu na masumbufu yetu; kwa kuwa mchana na usiku tulifanya kazi tusije tukamlemea mtu wa kwenu awaye yote, tukawahubiri hivi Injili ya Mungu. 1 THE. 2:9 SUV.
Unaona kwenye andiko hilo linavyosema, usiku na mchana Paulo na watumishi wenzake walifanya kazi za mikono ili wasije wakamlemea mtu. Kama ni hivyo unaweza ukaona ni jinsi gani ilivyo muhimu sana kujishughulisha na kazi ya mikono.
Ukiwa mchungaji, au nabii, au mwinjilisti, au mtume, au mwalimu, usione vibaya kujishughulisha, usione vibaya kulima mazao, usione vibaya kufunga ng’ombe, usione vibaya kuwa na kampuni yako, na mengine mengi ambayo sijayataja hapa.
Tusome Neno la Mungu kila siku, tutaweza kuyafahamu hayo maarifa, na itatusaidia kuelewa tunapaswa kufanya nini ili tusiwe mizigo kwa watu wengine. Na itakusaidia kuwa na hekima nyingi inayotokana na maarifa sahihi ya Neno la Mungu.
Mungu akubariki sana.
Ndugu yako katika Kristo,
Samson Ernest.
www.chapeotz.com