Mungu wetu anapenda yule mtu ambaye ameshamwamini, aishi kwa imani, imani ambayo inamwamini yeye kwa kila kitu, imani ambayo haitetereki, imani ambayo haina mashaka. Mtu anapoomba aamini atapokea kwa wakati wa Bwana, bila kujalisha muda, wala bila kujalisha mazingira.

Lakini inaweza ikawa tofauti siku za leo, kuwa unaweza kukutana na ndugu ambaye tayari ameokoka na Yesu ni Bwana na mwokozi wake. Imani yake mbele za Mungu inakuwa sio thabiti, nikiwa na maana kwamba bado ana wasiwasi au mashaka ndani yake juu ya utendaji wa Mungu.

Tunapaswa kujua katika vitu ambavyo Mungu wetu hapendezwi navyo ni mwenye haki wake, yaani yule ambaye tayari ameokoka, anakuwa na imani ya kusitasita. Hana ule uhakika kama Yesu aliye naye anaweza kumsaidia katika jambo lake gumu.

Wakati mwingine wapo ambao wamempa Yesu mipaka ya kuweza kuwasaidia kwenye baadhi ya shida zao, zipo shida anaona Yesu hataweza kumsaidia. Na zipo shida ambazo anaona kabisa Yesu Kristo ataweza kumsaidia.

Unafikiri mtu ambaye anaona kuna maeneo ambayo Yesu Anaweza kumsaidia, na kuna maeneo Yesu haiwezi kunisaidia. Unafikiri mwisho wake unakuwaje kwa mwamini wa namna hii, unaweza kuta ameanza kupata mawazo ya kutafuta msaada kwa miungu mingine.

Tena mwenye imani ya kusitasita anaweza akawa haamini kama Mungu yupo na upande mwingine anaamini yupo, mtu wa namna hiyo Mungu hawezi kuwa na furaha naye. Ikiwa upo upande haamini kama Mungu yupo, ujue kuna mahali atapeleka imani yake ambapo itakuwa ni chukizo kwa Mungu.

Hupaswi kuwa na imani ya kusitasita, imani isiyo na uhakika wa kupokea hitaji lako ulilomwomba Mungu, maana mwisho wake sio mzuri wa mwamini huyo. Na pia Neno la Mungu linasema hana furaha naye mwenye haki wake akiwa na imani ya kusitasita.

Rejea: Lakini mwenye haki wangu ataishi kwa imani; Naye akisita-sita, roho yangu haina furaha naye. EBR. 10:38 SUV.

Kuishi kwetu tunapaswa kuishi kwa imani, imani isiyo tetereka, na wala hatupaswi kuwa watu ambao wana kusitasita ndani yao juu ya Mungu. Hupaswi kabisa kuwa hivyo, na ukiwa mtu wa kusitasita, Mungu anasema hana furaha na wewe.

Tunajua maandiko yanatuambia imani huja kwa kusikia neno la Kristo, hakikisha unasoma neno la Mungu la kutosha, ili kuweka vizuri imani yako. Na kama hukuwa nayo kabisa imani, itajengeka kwako kupitia Neno la Mungu.

Ishi kwa imani na usiwe mtu wa kusitasita juu ya imani yako, naye Mungu atakuwa na furaha na wewe, Mungu akiwa na furaha na wewe itakuwa faida kubwa sana kwako ukiwa kama mtoto wake.

Mungu akubariki sana.
Ndugu yako katika Kristo,
Samson Ernest,
www.chapeotz.com