Tuna marafiki ambao wakati mwingine wanakuwa sio watu wazuri wa kuiga matendo yao wanayoyafanya, kwa kuwa ni marafiki zetu au kwa kuwa tunakuwa nao wakati mwingi. Tunaweza kujikuta tunaiga yale mabaya yao, bila hata sisi wenyewe kuelewa kama tumewaiga ubaya wao.

Ndio maana mtu makini na anayemjua Mungu hawezi kuwa na marafiki wabaya, kama anakuwa nao anakuwa nao makini, kwa kuwa bado tupo duniani. Hatuwezi kujitenga kabisa na watu wabaya, tutashirikiana nao baadhi ya vitu ila kwa mipaka.

Vile vile tunaweza tukawa na marafiki wazuri, marafiki ambao tunaweza kuiga mambo mazuri kutoka kwao, ule wema wao walionao, tunaweza kuiga na kufanya kama wao tena kwa viwango vizuri zaidi.

Vile wanavyoishi na watu na vile wanavyofanya mambo mbalimbali mazuri, hao ndio watu wa kuiga, tunaweza kuwafahamu kupitia njia mbalimbali ilimradi ni watu wazuri. Tunaweza kujifunza wema wao au ule uzuri wao.

Wapo watu waliotutangulia na wanaishi maisha mazuri ya mfano mzuri kwa wengine, sio vibaya tukajifunza kutoka kwao na kuiga mambo mazuri kutoka kwao. Kuliko kuiga ubaya kwa watu wasiomjua Yesu Kristo.

Rejea: Mpenzi, usiuige ubaya, bali uige wema. Yeye atendaye mema ni wa Mungu, bali yeye atendaye mabaya hakumwona Mungu. 3 YOH. 1:11 SUV.

Andiko hili linatupa dira na kutuhakikishia kuwa tunapaswa kuiga wema na sio ubaya, na yule anayetenda mabaya hakumwona Mungu au tunaweza kusema bado hajamjua Mungu sawasawa.

Katika maisha yako usije ukasahau hili, pamoja na kukutana na watu wa namna tofauti tofauti, hakikisha unaiga wema na sio ubaya. Yale mazuri yao ndio unapaswa kuiga, na yale mabaya yao unaachana nayo.

Hili liwe sehemu ya maisha yako, yale mazuri unayoweza kujifunza kwa mtu au kwa rafiki yako, au kwa ndugu yako, au kwa mzazi wako wa kiroho au kimwili, au kwa mtumishi yeyote yule utakayekutana naye kwenye maisha yako. Unapaswa kuiga wema wake.

Ukilizingatia hili maisha yako ya kiroho yatakuwa salama, maana unacho cha kuiga, ambacho ni wema, ubaya kwako utakuwa hauna nafasi kabisa katika maisha yako.

Mungu akubariki sana.
Ndugu yako katika Kristo,
Samson Ernest,
www.chapeotz.com