
Yapo mambo mengi sana mazuri ambayo tunasikia kutoka kwa watumishi mbalimbali wa Mungu, mambo ambayo yanatusihi tuenende katika njia sahih ya kumpendeza Mungu.
Wengine wazazi wetu wanatuelekeza tufuate njia sahihi na kujiepusha na njia zisizo sahihi, huwa hawaachi kutukumbusha kila wakati hasa pale wanapoona tunaonyesha kusahau.
Zipo njia nyingi sana zinazotumika kutuonya, kutuelimisha, na kutuelekeza yale tunayopaswa kuyafanya na tusiyopaswa kuyafanya katika maisha yetu ya wokovu.
Wengine tunapewa ujumbe moja kwa moja kupitia usomaji wa vitabu mbalimbali vya watumishi wa Mungu, wengine kupitia usomaji wa Neno la Mungu.
Pamoja na kuwa wasikiaji sana wa Neno la Mungu kupitia mafundisho mbalimbali na kupitia usomaji wetu wenyewe, utakuta bado ipo shida kubwa kwa walio wengi.
Wengi tunasikia mafundisho mbalimbali mazuri ila tunakuwa kama watu ambao hawajasikia kabisa hayo mafundisho, yaani tunakuwa hatuna tofauti na yule ambaye hajasikia chochote kile.
Tunapaswa kuwa wasikiaji wa Neno, na watendaji wa Neno, yale mafundisho unayoyasikia yatakuwa na faida kubwa kwako, kiroho na kimwili, na mwisho wake utaurithi ufalme wa Mungu.
Rejea: Yeye aliye na sikio, na alisikie neno hili ambalo Roho ayaambia makanisa. UFU. 3:6 SUV.
Mungu haletii ujumbe wake bure kwa kanisa lake, kila ujumbe una maana yake na unapaswa kuushika na kuutendea kazi, ukibaki kuwa mtu wa kusikia na kupuuza hiyo bado sio kusikia.
Yule anayesikia ndiye anayetenda kama alivyosikia, ndivyo tunayopaswa kuwa wana wa Mungu, tukiwa wasikiaji na watendaji wa Neno tutakuwa salama kabisa.
Rejea: Lakini iweni watendaji wa neno, wala si wasikiaji tu, hali mkijidanganya nafsi zenu. YAK. 1:22 SUV.
Mungu akusaidie uwe msikiaji na mtendaji wa yale yanayompendeza Mungu, yale yasiyompendeza Mungu achana nayo kabisa ili maisha yako yabaki kuwa safi mbele za Mungu.
Mungu akubariki sana.
Ndugu yako katika Kristo,
Samson Ernest,
www.chapeotz.com