Tuingie moja kwa moja kwenye mada tajwa hapo juu, watu baadhi wameingia kwenye ndoa na watu sahihi ila mitazamo yao juu yao sio sahihi, wapo wameingia kwenye ndoa sio sahihi kwa sababu ya mitazamo yao isiyo sahihi, na wapo hawataki kuingia kwenye ndoa wamebaki kutangatanga na kila mwanaume/mwanamke kwa sababu ya mitazamo yao mibaya.
Mtu anaweza akawa anatamani sana ya kupata mtu sahihi wa kuishi naye ila akawa ana mtazamo hasi juu ya wanaume au wanawake, mtu huyu akiingia kwenye ndoa anaweza asiifurahie kwa sababu hii; kila atakachokosea mke/mume wake atakuwa anamkumbushia kuwa “wanawake/wanaume ndio tabia zenu au ndivyo mlivyo”.
Wengine wana mtazamo kuwa “wanaume huwa hawaridhiki na mwanamke mmoja” wengine “wanawake wote mama yao ni mmoja”, wengine wanaamini wa “kumwamini ni mama yako mzazi tu” yaani wengine hawapaswi kuaminiwa. Nje kabisa na neno la Mungu.
Unakutana na kijana wa kiume ana mtazamo mbaya juu ya mabinti, kila atakayekutana naye anamchukulia kama chombo Fulani cha starehe au kisicho na thamani. Vijana wa namna hii wakipata nafasi ya kufanya uasherati na binti, mara nyingi mabinti hao huishia kuachwa.
Mabinti wengine wamejenga mtazamo wao kwenye vitu, kila mwanaume atakayekuja kwao kipaumbele chao kikubwa ni ana nini? Ana mali za kutosha? Wanasahau kuangalia mambo ya msingi, wanapoingia kwenye ndoa wanakutana na changamoto ngumu.
Kuangalia mafanikio ya kimwili sio jambo baya, ila ukilipa kipaumbele kwenye uchaguzi wako unaweza kusahau kuangalia vitu vya muhimu vitakavyokufanya ufurahie ndoa yako. Na ukiwa na mtazamo kuwa asiye na kitu atakufaa napo unaweza kuingia kwenye mahusiano yasiyo sahihi.
Jambo kubwa tunalozungumza hapa ni kubadili mtazamo wako hasi juu ya ndoa au wanaume au wanawake, inawezekana umekutana na matukio mengi ya kukuumiza, bado unapaswa kuwa na Imani kuwa kuna watu wema duniani.
Unaweza kufikiri dunia haina watu wazuri, ukawa na mtazamo kuwa wanaume waaminifu na wanaopenda wake zao sawasawa walikuwa wa zamani na sio wa sasa, unaweza kufikiri kuwa wanawake waaminifu na wanaojali waume zao walizamaga na meli!
Ukiingia kwenye ndoa na mtazamo mbaya juu ya wanaume/wanawake, uwe na uhakika utakutana na changamoto ngumu ambazo zimesababishwa na vile vitu ulivyoviumba kwenye ufahamu wako.
Dunia ya sasa ina mambo ya ajabu mengi na watu wa ajabu ila unapaswa kufahamu bado watu wema wapo, bado wapo watu wanaomcha Bwana katika Roho na kweli, watu waliojaa hofu ya Mungu, watu wasio na utani na mambo ya Mungu.
“Bwana, wamewaua manabii wako, wamezibomoa madhabahu zako, nami nimesalia peke yangu, nao wananitafuta roho yangu. Lakini ile jawabu ya Mungu yamwambiaje? Nimejisazia watu elfu saba wasiopiga goti mbele ya Baali. Basi ni vivi hivi wakati huu wa sasa, yako mabaki waliochaguliwa kwa neema”, Rum 11:3-5 SUV.
Hali kama hii ilimkuta Eliya kama tulivyoona kwenye maandiko, alijiona amebaki peke yake, lakini jibu la Mungu lilikuwa tofauti na alivyokuwa anafikiri au anawaza. Ndivyo ilivyo hata sasa, Mungu anayo mabaki ya kutosha ya watu wake. Omba Mungu akukutanishe na mtu sahihi kwako.
Usiwe na mitazamo mibaya kama watu wasioamini Mungu wa kweli, uwe na mtazamo mzuri wa Kimungu, maana wewe unaye Yesu moyoni mwako na Roho Mtakatifu ni kiongozi wako, usijione wewe umebaki peke yako unayemcha Mungu katika Roho na kweli.
Ukishakuwa na mtazamo sahihi alafu ukawa unahitaji kuoa au kuolewa, uwe na uhakika ukitulia mbele za Mungu sawasawa na ukamwomba mwenzi wa maisha yako, atakupa mtu sahihi na anayefanana na wewe.
Upo kwenye ndoa badili mtazamo wako mbaya ndipo uendelee kumwomba Mungu akusaidie juu ya changamoto unazokutana nazo kwenye ndoa yako. Kama bado hujaingia kwenye ndoa nawe badili mtazamo wako haraka, tena wewe una fursa kubwa sana ya kurekebisha mengi kabla ya kuingia kwenye ndoa.
Soma neno ukue kiroho na penda mafundisho ya neno la Mungu, ili mtazamo wako ubadilike na uanze kuona mambo kwa namna ya tofauti na njema.
Mungu akubariki sana
Samson Ernest
+255759808081