
Katika vitu ambavyo hupaswi kuyumbishwa navyo ni pale unapojua kile unachopanda katika maisha yako, kama unapanda mema uwe na uhakika utavuna matunda ya wema wako.
Leo unapanda kwa machozi mengi kweli ila unapaswa kufahamu wakati wako wa kuvuna matunda ya kile ulichokipanda utafika, haijalishi utachukua muda mrefu sana. Kama unapanda mema uwe na uhakika utavuna matunda ya wema wako.
Wakati mwingine huwa tunafika tunaacha kutenda wema wetu, kile ambacho tulikuwa tunakifanya na kinaleta matunda mazuri kwa wale tuliokuwa tunawatendea. Huwa tunaacha kutokana na sababu za kidhaifu kabisa ambazo zimeturudisha nyuma.
Leo unaweza ukawa unapanda kwa machozi mengi kwa watoto wako, unapambana kuhakikisha watoto wako wanapata malezi bora. Unahakikisha watoto wako wanakuwa na bidii katika kumjua Yesu Kristo, hata kama hawakuelewi sana. Uwe na uhakika hicho unachofanya kwa watoto wako utavuna matunda ya kazi unayofanya kwa watoto wako.
Unafanya huduma ya kumtumikia Mungu, unafika mahali unaona kama vile kile unachokifanya hakikuzalishi matunda mazuri sana ya kukutia moyo, bali unaona unaambulia mambo ya kukuumiza moyo wako. Pamoja na mabaya unayokutana nayo kwenye huduma yako, uwe na uhakika utavuna matunda ya kazi yako kwa nyimbo za shangwe au kwa kelele za furaha.
Ikiwa unafanya kitu ambacho hakimkosei Mungu wako, bali kinamletea sifa na utukufu, au kinawafanya wengine wawe vizuri, au kinawavuta watu kwa Yesu Kristo, au kinawafanya watu waone na wao wanapaswa kuendelea kuishi duniani. Fahamu kwamba utavuna matunda ya kazi yako kwa nyimbo za shangwe.
Unaweza ukawa unajiuliza mbona unakutana na vita vikali sana, ama inawezekana unajiuliza itakuwa lini kuvuna matunda ya kile unakifanya? Maana ukiangalia mambo unayokutana au yanayokukabili mbele yako, unaona ni mambo mazito sana.
Pamoja na mambo magumu unayokutana nayo, cha kuzingatia sana ni kuendelea kuishi maisha yanayompendeza Mungu, ni kuendelea kuishi katika msingi wa Neno la Mungu. Itafika saa utavuna matunda ya kile ulikuwa unapanda.
Nimeipenda Biblia ya Neno, biblia hii ya kiswahili cha kisasa inafafanua vizuri sana huu mstari ninaoenda kukushirikisha. Hasa kwa mtu anayepanda kwa machozi, inasema wakati wa kuvuna kwake atavuna kwa nyimbo za shangwe.
Rejea: Wapandao kwa machozi watavuna kwa nyimbo za shangwe. Zaburi 126:5 NEN.
Kwanza tunachokiona kwenye huu mstari unatuhakikishia kwamba mtu yeyote anayepanda kwa machozi, wakati wake wa kuvuna kile alichokipanda upo. Hilo ni jambo la msingi sana kuzingatia sana kwa wewe mpandaji.
Jambo lingine la pili tunaliona kwenye mstari huu ni nyimbo za shangwe, huyu mpandaji aliyepanda kwa machozi, saa yake ya kuvuna ikifika hatavuna kimya kimya. Nyimbo za shangwe zitasikika kwake, wakati ambao inakuwa ngumu kujizuia maana Mungu ametoa matokeo mazuri ya mpandaji huyu.
Angalia ni jambo gani unapanda leo kwenye maisha yako, hapa tumeona uzuri wa kupanda mambo mazuri, kama unapanda mambo mabaya. Nasikitika kukuambia kuwa utavuna matunda ya ubaya wako, hata kama sasa hivi unafurahia ubaya unaofanyia wengine.
Je, saa yako ya kuvuna ulichokipanda ikifika una uhakika utavuna kwa nyimbo za shangwe au utavuna kwa kilio kikubwa cha maumivu makali? Kama unapanda mema uwe na amani ila kama unapanda mabaya rekebisha haraka hilo, maana saa ya mavuno utalia.
Huenda ulifika mahali ambapo uliona huna haja ya kuendelea kupanda mambo mazuri kwenye eneo ambalo ulikuwa unapanda, eneo ambalo baadaye ungeshangilia wakati wa mavuno. Kupitia ujumbe huu rudi tena kwenye eneo lako la kupanda, ili saa ya mavuno itakapofika uvune kwa nyimbo za shangwe.
Hii ndio faida ya kusoma Neno la Mungu, unapata nafasi ya kujua kile kizuri unafanya kina faida yake, japo kwa wakati huo unaweza usione sana uzuri wake. Upo wakati wa mavuno, wakati ambao utakufanya uimbe nyimbo za shangwe.
Mungu akubariki sana.
Ndugu yako katika Kristo,
Samson Ernest,
www.chapeotz.com
+255759808081