
Moto wa kuni utaendelea kuwaka muda mrefu bila kuzimika kama aliyewasha ule moto, ataendelea kuchochea kuni na kuongeza pale kuni zitakapoisha au zitapopungua. Huo moto utaendelea kuwaka bila kuzimika wenyewe, ila kama utakosa mtu wa kuuchochea utazimika wenyewe.
Ndivyo ilivyo na karama za Mungu tulizonazo ndani yetu, bila kuendelea kuzichochea kila wakati, taratibu zitaendelea kupoa na mwisho wa siku zinapotea kabisa. Inabakia hadithi tu kuwa fulani alikuwa ana karama kubwa sana.
Ndugu, ikiwa Mungu ameweka karama ndani yako ili umtumikie yeye, ama ikiwa watumishi wa Mungu wamekuwekea mikono kwa ajili ya huduma uliyopewa na Mungu. Usije ukaacha kuchochea karama yako, mikono uliyowekewa na watumishi wa Mungu haimaanishi kwamba itakufanya usipoe.
Juhudi zako za kuendelea kujifunza neno la Mungu, kuhudhuria mafundisho ya neno la Mungu, kuwa na muda wa kuomba Mungu, kuwa na muda wa kujifunza kwa watumishi wengine kwa njia ya vitabu vyao, au kwa njia ya DVD/CD zao.
Kufanya hivyo kutakufanya uendelee kuichochea karama iliyo ndani yako, ukikaa tu bila kujishughulisha, au bila kuweka bidii kwa kile Mungu amekupa ndani yako. Unaweza kushangaa umri umekutupa mkono na hakuna ulichomzalia Mungu matunda.

Mtumishi wa Mungu mwenye karama ndani yako, hakikisha unaichochea karama yako, usiangalie sana hali duni uliyonayo kwa sasa. Tafuta kuichochea karama yako kila siku wakati, hichi ni cha msingi sana sana kwenye utumishi wako.
Rejea: Kwa sababu hiyo nakukumbusha, uichochee karama ya Mungu, iliyo ndani yako kwa kuwekewa mikono yangu. 2 TIM. 1:6 SUV.
Vile Mungu alikutumia jana, usijisahau na kujiona huna haja ya kujishughulisha zaidi, hapa tunaona mtume Paulo anamhimiza Mtoto wake wa kiroho Timotheo kuhusu kuichochea karama yake.
Inaonyesha ni jinsi gani ilivyo na umhimu wa kuichochea karama yako, bila kufanya hivyo maana yake ile karama iliyo ndani yako inapoa. Na ikishapoa hakuna cha tofauti utakachofanya kwenye utumishi wako, maana kile alichokupa Mungu ndani yako hakina nguvu tena.
Chochea karama yako, maadam una karama ndani yako uliyopewa na Mungu, ichochee haswa kwa nguvu zako zote, hata kama huoni sana vile viwango ambavyo Mungu amekuahidia. Endelea kuchochea karama yako kila wakati, usije ukaacha hili, ukiacha tu unapotea.
Hii ndio faida ya kusoma Neno la Mungu kila siku, unakutana na neno lako litakalokusudia kwenye utumishi wako, ama kwenye maisha yako ya wokovu, ulifika mahali ukachoka. Neno la Mungu linakuhuisha tena na kujisikia nguvu mpya za kuendelea kusonga mbele zaidi.
Mungu akubariki sana.
Ndugu yako katika Kristo,
Samson Ernest,
www.chapeotz.com