
Kukosa maarifa sahihi muda mwingine imetufanya tumkosee Mungu pasipo wenyewe kujua kama tunamkosea, wengi wetu tumekuwa tukisema hatuwezi kuwanyenyekea binadamu wenzetu. Tunaona wa kumnyenyekea ni Mungu peke yake, bila kujua kuwa tunaweza kumnyenyekea mtu na tusimkosee Mungu wetu.
Wakati mwingine tumekosa kabisa adabu kwa watawala na wenye mamlaka, kwa kufikiri tupo sahihi kwa kufanya hivyo, bila kujua kuwa tunapaswa kuwanyenyekea watawala na kuwatii wenye mamlaka.
Kumnyenyekea mtawala yeyote ni muhimu sana na kumtii mwenye mamlaka yeyote ni muhimu sana kwako ukiwa upo chini yake, au unaweza usiwe unaongozwa naye ila unapaswa kumnyenyekea na kumtii.
Hili tunaweza tukawa hatulichukulii kwa uzito sana kutokana na dhana mbovu juu ya watawala na wenye mamlaka, huenda mapokeo tuliyonayo ndio yametufanya tuwaone watawala na wenye mamlaka sio kitu kwetu.
Hata ile heshima yao tunakuwa tunaipuuza na kuona hawastahili kupewa na sisi, tunakuwa tunaonyesha dharau kwao, tunakuwa tunawatukana vile tunavyoweza kufanya hivyo.
Kukosa adabu kwa watawala na wenye mamlaka sio kana kwamba tunakuwa tunafanya vizuri sana, kufanya hivyo inakuwa sio sahihi kwa mtu aliyeokoka. Anakuwa anatenda kosa ambalo anapaswa ajirekebisha, bila kujirekebisha anakuwa na hatia mbele za Mungu.
Ukiwa unasoma ujumbe huu, acha kuwachukulia watawala na wenye mamlaka kama watu ambao hawapaswi kupewa heshima yao, kuanzia sasa kupitia maandiko haya ninayoenda kukushirikisha hapa uwe unawapa watawala na wenye mamlaka heshima yao.
Rejea: Wakumbushe watu kuwanyenyekea watawala na kuwatii wenye mamlaka, wawe tayari kutenda kila lililo jema. Wasimnenee mtu yeyote mabaya, wasiwe wagomvi, bali wawe wapole, wakionyesha unyenyekevu kwa watu wote. Tito 3:1-2 NEN.
Umeona hiyo mistari inavyosema? Tunapaswa kuwanyenyekea watawala na kuwatii wenye mamlaka, kama huna utaratibu huo unapaswa kuwepo kuanzia sasa. Maandiko yanatuasa tuwe hivyo, kwahiyo hatuwezi kupuuza haya na kuendelea kuishi tunavyotaka sisi.
Tena sio wenye mamlaka tu, ni kwa watu wote tunapaswa kuonyesha unyenyekevu mkubwa kwao, hatupaswi kuwadharau na kuwachukulia kawaida. Wanapaswa kupewa heshima yao kutokana na umri wao au nafasi zao.
Mwongozo wa maisha yetu kama wakristo upo ndani ya biblia, hatuwezi kuipuuza hata siku moja, haijalishi inaenda kinyume na mapokeo ya dini zetu. Tunapaswa kuishi kile ambacho tunaelekezwa na maandiko matakatifu, bila kufanya hivyo tutapotea njia.
Mtu yeyote atakayechaguliwa kuwa mtawala unapaswa kumnyenyekea, na mtu yeyote yule atakayekuwa mwenye mamlaka unapaswa kumtii. Sio kwa kinafiki ni ile kutoka ndani ya moyo wako ukiwa unajua unaenda sawasawa na maandiko yanavyosema.
Isipokuwa haipaswi kuchukua nafasi ya Mungu, maana wapo wanaweza kutumia hili kama mwanya wa kuabudiwa wenyewe, badala utukufu kumrudia Mungu. Wao wanakuwa wanauchukua wao, wakifanya hivyo wawe na uhakika watamkasirisha Mungu.
Hii inakuhimiza kuendelea kujifunza zaidi Neno la Mungu, hakikisha unaweka ratiba yako vizuri katika kusoma Biblia yako. Utajifunza mambo mengi sana yanayoweza kukusaidia katika maisha yako ya wokovu, utaenda kama mtu mwenye hekima nyingi.
Mungu akubariki sana.
Ndugu yako katika Kristo,
Samson Ernest,
www.chapeotz.com
+255759808081