“Maana unabii haukuletwa po pote kwa mapenzi ya mwanadamu; bali wanadamu walinena yaliyotoka kwa Mungu, wakiongozwa na Roho Mtakatifu”, 2 Pet 1:21 SUV.
Petro anatuthibitishia wazi asili ya Kimungu na mamlaka yake ya unabii kwenye Maandiko Matakatifu.
Waamini wote wanapaswa kuwa na mtazamo usiobadilika kuhusu maandiko matakatifu yaliyovuviwa na yaliyojaa mamlaka ya Kimungu.
Ukishasoma neno la Mungu unapaswa kumhuruhusu Roho Mtakatifu akufundishe kile ambacho unapaswa kukielewa.
Ujumbe usiokuwa na mashaka kwa kanisa au waamini ni ule unaotokana na neno la Mungu.
Tunaposema kuna Roho Mtakatifu tujue yupo roho mwingine mpotoshaji, bila kuwa na neno la Mungu sahihi hutaelewa hili.
Mtu asiye na kweli sahihi ya neno, mtu asiye na Roho wa Mungu ndani yake, vigumu kutofautisha haya. Akiambiwa ujumbe huu unatoka kwa Mungu ataupokea kama ulivyo.
Tunapaswa kuelewa hatupaswi kunena neno la Mungu kwa mawazo yetu, tunapaswa kuwa na mtazamo sahihi kupitia maandiko matakatifu.
Tukiwa hatuna mtazamo imara kupitia neno la Mungu tuwe na uhakika kuwa hatutakuwa na mafundisho sahihi.
Mtazamo sahihi wa neno la Mungu, unatupa fursa wa kuweza kufundisha na kuhubiri injili sahihi na yenye kubadilisha maisha ya watu.
Roho Mtakatifu hutumia vinywa vyetu kusema na watu, Mungu anaweza kusema na waamini au watu kupitia ujumbe wa neno la Mungu.
Mungu amekuamini, hakikisha unatumia mamlaka aliyokupa kufikisha ujumbe sahihi kupitia maandiko matakatifu.
Wanaopotosha maandiko matakatifu ni wengi ila hupaswi kupoteza muda mwingi kuhangaika nao, tumia muda mwingi kuifundisha kweli na neno la Mungu.
Soma neno ukue kiroho
Liwe jua iwe mvua soma biblia yako
Mungu akubariki sana
Samson Ernest